Pages

Friday, May 1, 2015

Ukawa wakuna vichwa saa 48

Mwenyekiti  mwenza wa Ukawa, Freeman Mbowe akizungumza wakati wa mkutano na waandishi  wa habari, Dar es Salaam jana. Wengine ni wenyeviti wenza,James Mbati,  Profesa Ibrahim Lipumba na  Dk Emmanuel Makaidi. Picha na Said Khamis 
Na Joyce Mmasi na Kelvin Matandiko, Mwananchi
Kwa ufupi
  • Vyama hivyo vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi vimekubaliana kusimamisha mgombea mmoja kuanzia kiti cha urais hadi udiwani, lakini kazi ya kugawana majimbo imekuwa ikivisumbua na ilitarajiwa kuwa ingemalizika juzi baada ya viongozi kukutana kwa siku mbili kuanzia Jumanne.

Dar es Salaam. Saa 48 zilizotumika kikaoni kutafuta muafaka wa majimbo yenye utata ndani ya umoja wa vyama vya upinzani vilivyo chini ya Ukawa, zimekatika bila mafanikio na  mvutano unaonekana kubakia kwenye majimbo 12 kati ya 239 waliyopanga kugawana.
Vyama hivyo vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi vimekubaliana kusimamisha mgombea mmoja kuanzia kiti cha urais hadi udiwani, lakini kazi ya kugawana majimbo imekuwa ikivisumbua na ilitarajiwa kuwa ingemalizika juzi baada ya viongozi kukutana kwa siku mbili kuanzia Jumanne.
Lakini habari kutoka ndani ya kikao hicho kilichofanyika jijini Dar es Salaam zinaeleza kuwa wajumbe walishindwa kufikia muafaka kwenye majimbo 12.
Hata hivyo, viongozi hao wa vyama hivyo walikataa kutaja majimbo hayo yaliyosalia.
Wakizungumza na waandishi wa habari kwenye ofisi za makao makuu ya CUF, viongozi wa vyama vinne vinavyounda Ukawa, James Mbatia (NCCR-Mageuzi), Freeman Mbowe (Chadema), Profesa Ibrahim Lipumba (CUF) na Emmanuel Makaidi (NLD) walisema tayari wamefikia muafaka katika majimbo 227 kati ya majimbo 239 yaliyopo nchini.
“Tangu juzi tupo hapa tukijadili namna ya kuwapata wagombea wa Ukawa wa ngazi zote za udiwani, ubunge na urais. Kwa kiasi kikubwa tumekamilisha kazi ya kupata wagombea ubunge kwa zaidi ya asilimia 95 ya majimbo yote ya uchaguzi, majimbo 12 yaliyobaki tunaendelea kuyashughulikia na tutayapatia ufumbuzi muda si mrefu,” alisema Mbatia aliyezungumza kwa niaba ya wenyeviti wenzake.
Viongozi hao, kila mmoja kwa nyakati tofauti, walijigamba kuwa umoja wao huo upo imara na kwamba wale wanaopiga ramli kuwa utavunjika, wataendelea kusubiri lakini kamwe jambo hilo halitatokea.
Mbowe
Mwenyekiti mwenza wa umoja huo, Mbowe alisema hatua iliyofikiwa kwa sasa inatia matumaini ya kufanikiwa kwa mpango wa kusimamisha mgombea mmoja wa ubunge, udiwani na urais.
“Kwa wale wanaopiga ramli ya kuvunjika kwa Ukawa hawatafanikiwa. Tutasimamisha mwakilishi mmoja kuanzia udiwani, ubunge mpaka urais. Tunajua hitaji la Watanzania kwa sasa ni kuwaondoa kwenye kifungo cha CCM,” alisema Mbowe.
Alipoulizwa kuhusu mvutano wa majimbo hayo 12, Mbowe alisema siyo jambo la kushangaza kwa vyama vinne kutovutana katika mgawanyo wa majimbo hayo kwani kila chama kinajiamini na kinahitaji kupata mwakilishi.
“Tuko vyama vinne,  itakuwa ajabu kama mvutano utakosekana, lakini tumepata asilimia 95. CCM wenye chama kimoja hawajatangaza mgombea hata mmoja.”

No comments:

Post a Comment