Mtendaji Mkuu wa Wakala wa
Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA), Mhandisi Victor Seff akiwa
kwenye kikao kazi na Waratibu wa TARURA wa Mikoa, kwenye kikao
kilichofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa TARURA Makao Makuu- Mtumba
jijini Dodoma hivi karibuni.
……………………………………………………………………………………………….
Na. Erick Mwanakulya
Mtendaji Mkuu wa
Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA), Mhandisi Victor Seff
amewataka Waratibu wote wa TARURA nchini kufanya ukaguzi wa mara kwa
mara
katika barabara na madaraja ili kubaini maeneo yanayohitaji
ukarabati na kuyafanyia kazi kabla ya kuleta madhara.
Mhandisi Seff
ameyasema hayo, alipokutana na Waratibu wa TARURA wa Mikoa jijini Dodoma
katika ukumbi wa Mikutano wa Ofisi za TARURA Makao Makuu zilizopo
Mtumba, ikiwa ni sehemu ya kikao kazi kilicholenga kutoa maelekezo na
miongozo mbalimbali ya ufanyaji kazi ili kuwapatia wananchi huduma ya
usafiri na usafirishaji.
Aidha, Mtendaji
Mkuu amesisitiza kuwa, ukaguzi wa mara kwa mara wa miundombinu unasaidia
kupunguza gharama kwani uharibifu au uchakavu wa miundombinu ukibainika
mapema ukarabati wake unaweza kufanyika katika hatua za awali kwa
gharama nafuu na kwamba miundombinu inapoharibika moja kwa moja gharama
inakuwa kubwa sana pale inapobidi kujengwa upya.
Pia, Mhandisi
Seff amesisitiza juu ya uwekwaji wa alama za barabarani hasa katika
maeneo maalumu kama madaraja na maeneo yaliyoharibika ili watumiaji wa
barabara watambue vizuri maeneo hayo wakati wa kupita.
‘‘Natoa maelekezo
juu ya uwekwaji wa alama za barabarani kwamba, hakikisheni mnaweka
alama za kudumu maana sitamsikiliza yeyote atakayekuja na sababu kuwa
kibao kimeibiwa wakati angeweza kuweka kibao cha kudumu hata kwa kutumia
zege maana bila kuwa na alama hizo inaweza kuwa chanzo cha ajali”,
amesisitiza Mhandisi Seff.
Ili kurahisisha
usimamizi wa kazi kwa mikoa yote kiongozi huyo ameeleza kuwa, anaendelea
kutoa magari kwa Waratibu wote wa TARURA na kisha atatoa magari kwa
Mameneja wa TARURA wa Halmashauri ili kuhakikisha wanasimamia kazi na
wananchi wanasafiri kwa urahisi.
Wakala wa
Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) unaendelea kutekeleza majukumu
yake katika Mji wa Serikali Mtumba baada ya kukamilisha ujenzi wa ofisi
yake na kuhamia rasmi.
No comments :
Post a Comment