*******************************
Halmashauri ya Manispaa ya
Kinondoni imeendelea kupambana vikali kuthibiti kuenea kwa virusi vya
COVID 19 (Corona) kwa kupuliza dawa katika hotel za kitalii zilizopo
katika Halmashauri hiyo.
Hatua hiyo ni muendelezo wa
mkakati uliowekwa na Mkuu wa Wilaya hiyo Mhe. Daniel Chongolo,
Mkurugenzi Aron Kagurumjuli, Mstahiki Meya Benjamini Sitta, pamoja na
Mganga mkuu Samweli Laizar kwa pamoja, katika kuhakikisha kuwa
maambukizi ya Virus hivyo hayasambai kwa wananchi na hivyo wanaendelea
kuwa salama.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo
Kaimu Mganga mkuu wa Kinondoni, Dk. Said Hemed amesema kuwa lengo ni
kuhakikisha kuwa wananchi wanakuwa salama katika kuepukana na maambukizi
ya magonjwa ya mlipuko.
Amefafanua kuwa mbali na kuthibiti
maambukizi ya virusi vya Corona, lakini pia wanachukua tahadhari ya
mlipuko wa homa ya dengu kwakuwa hivi sasa ni kipindi cha mvua.
Ameongeza kuwa kupuliza dawa
katika maeneo hayo ni mahususi kwakuwa wageni wengi hufikia katika
hoteli hizo na kwamba wataendelea kuthibiti kwenye maeneo mbalimbali ili
virusi hivyo visienee kwenye makazi ya wananchi.
“ Tunapopuliza hizi dawa ni kwa
malengo mawili, kwanza tunathibiti Corona isisambae lakini pia
tunathibiti homa ya dengue, ukiangalia kipindi hiki ni cha msimu wa
mvua, magonjwa mengi ya mlipuko hutokea , kwa hiyo hii ni njia ya
kuwakinga wananchi wetu wa Kinondoni wasipate maambukizi yoyote” amesema
Dokta Hemed.
Aidha ameongeza kuwa” hotel hizi
za kitalii ni maarufu na ndio ambazo zinapokea wageni wengi, niwasishi
sana waendelee kuchukua tahadhari kwakutoa ushirikiano na Halmashauri
yetu ili mlipuko huu usiendelee kwenye maeneo watu.
Awali Kinondoni ilianza mchakato
huo wa kupuliza dawa katika vituo vya daladala, mwendokasi, na maeneo
yenye mikusanyiko ya watu ikiwemo Kanisani na Misikitini pamoja na
maeneo ya wananchi na kwamba bado zoezi hilo linaendelea.
Hadi sasa zoezi la utoaji elimu
kwa wananchi wa Kinondoni linaendelea kwani Kata 20 zilizopo kwenye
Halmashauri zimeshafikiwa sambamba na matangazo ikiwemo kubandika
mabango, kugawa vipeperushi kwa wananchi vyenye ujumbe wa kuelimisha
namna ya kujikinga na virusi vya COVID19 ( Corona).
No comments :
Post a Comment