Friday, April 3, 2020

JUHUDI ZA WIZARA YA MADINI KUFUNGUA MASOKO YA MADINI YASABABISHA WACHIMBAJI WADOGO KUVAMIA MAENEO YA MIGODI MIDOGO[RUSH]


……………………………………………………………………………………..
Na.Alex Sonna,Dodoma
Bunge limeelezwa kuwa ,Kutokana na juhudi kubwa zinazofanywa na Wizara  ya Madini katika kutenga maeneo kwa ajili ya wachimbaji wadogo na kufungua masoko ya madini nchi nzima, kumesababisha ongezeko la wachimbaji wadogo ambao wamekuwa wakivamia maeneo
mbalimbali ya Migodi midogo (rush) .
Taarifa hiyo imetolewa leo  Bungeni jijini Dodoma  kutoka wizara ya Madini kwa njia ya Maandishi  wakati  Wizara hiyo ikijibu swali la Mbunge  wa viti Maalum Salome Makamba aliyehoji  Je, ni sifa zipi ambazo mzabuni anatakiwa kuwa nazo ili kupewa nafasi ya usimamizi mapato ya Serikali kwenye migodi midogo midogo (Rush) kama Mwabomba, namba Mbili, Segese.
 Katika Majibu ya Wizara ya Madini imefafanua kuwa maeneo ambayo yanavamiwa zaidi na wachimbaji wadogo   ni yale yaliyotengwa, maeneo yenye leseni kubwa za utafiti, maeneo ya uchimbaji mkubwa, maeneo yasiokuwa na leseni, na maeneo ambayo leseni zake hazijaendelezwa kwa shughuli za uchimbaji.
Aidha Majibu ya wizara hiyo yameendelea kufafanua kuwa ,Serikali kupitia Tume ya Madini ilitoa Waraka wa Ndani Na. 3 ulioanza kutumika tarehe 15 Oktoba, 2019 wenye dhumuni la kutoa mwongozo kwa Maafisa Madini Wakazi na watumishi wengine katika kusimamia, kudhibiti shughuli za madini na mapato ya Serikali katika maeneo yenye  Migodi  midogo[rush.]
 Kwa mujibu wa Waraka huo, utaratibu unaotumika kuwapata wasimamizi wa rush ni kupitia Kamati ya Uongozi inayofuatilia na kuimarisha usimamizi katika eneo la rush.
 Majibu ya Wizara ya madini yameendelea kubainisha kuwa ,Kamati hiyo huteua Wasimamizi wa migodi midogomidogo[ rush], ambapo Mwenyekiti wa rush anapaswa kuwa na sifa zifuatazo:- Awe mchimbaji mzoefu hasa katika usimamizi wa maeneo ya aina hiyo; Asiwe na historia ya wizi wa fedha za Serikali; na Awe mwaminifu.
Aidha, wajumbe wengine kwenye usimamizi wa rush ni pamoja na Katibu, Mweka Hazina, M/kiti wa Kijiji, M/kiti wa Kitongoji, Mjumbe wa REMA, TAWOMA na Mwakilishi wa eneo/shamba.

No comments :

Post a Comment