Mkurugenzi wa Tiba Shirikishi
ambaye pia ni Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kutoka Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete (JKCI) Delila Kimambo akielezea jinsi mashine ya kupima
moyo (Echocardiogram) inavyofanya kazi ya kutambua matatizo yaliyopo
katika moyo wakati wa mkutano wa kwanza wa kitaifa wa kutathmini
magonjwa ya moyo nchini uliofanyika leo katika ukumbi wa mikutano wa
JKCI uliopo Jijini Dar es Salaam.
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo
kutoka Shirika la Madaktari Afrika la nchini Marekani Prof.Matthew
Sackett akielezea jinsi mtambo wa Cathlab unavyotumika kutibu na
kupima magonjwa ya moyo wakati wa mkutano wa kwanza wa kitaifa wa
kutathmini magonjwa ya moyo uliofanyika leo katika ukumbi wa mikutano
wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) uliopo jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya Madaktari wa Magonjwa ya
Moyo kutoka Hospitali mbalimbali za mkoa wa Dar es Salaam
wakifuatilia mada ya jinsi ya kumtambua mgonjwa mwenye matatizo ya moyo
kwa kupitia kipimo cha ECHO wakati wa Mkutano wa kwanza wa kitaifa wa
kutathmini magonjwa ya moyo nchini uliofanyika leo katika ukumbi wa
mikutano wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) uliopo jijini Dar es
Salaam.
Na Salome Majaliwa – JKCI
17/08/2018 Madaktari wa Hospitali za Rufaa nchini wameshauriwa kuwatuma mapema wagonjwa wa moyo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) pindi wanapowapima na kugundulika kuwa na ugonjwa huo ili waweze kupatiwa matibabu mapema.
Rai hiyo imetolewa leo na Mkurugenzi wa Tiba Shirikishi ambaye pia ni Daktari bingwa wa magonjwa ya Moyo kutoka JKCI Delila Kimambo wakati wa mkutano wa kwanza wa kitaifa wa kutathmini magonjwa ya moyo nchini uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Taasisi hiyo.
Dkt. Delila alisema wagonjwa
wa moyo wanaotibiwa katika Hospitali mbalimbali hapa nchini rufaa yao
huwa ni Taasisi ya Moyo hivyo basi ni muhimu wagonjwa hao wakafika
katika Hospitali hiyo kwa wakati.
“Wagonjwa wengi tunaowapokea mioyo yao huwa imechoka, kama wagonjwa hawa wangefika mapema kwetu wangepata matibabu madogo kuliko kupatiwa matibabu makubwa ya upasuaji wa kifua au bila kufungua kifua kwa kutumia tundu dogo”.
“Kutokana
na wagonjwa wengi kuchelewa kufika hospitalini ama kutokupata matibabu
ya moyo kwa wakati, tumeona tuwe na mafunzo haya hii itawasaidia madaktari wengi kupata ujuzi zaidi na kuweza kutambua wagonjwa kwa wakati”, alisema Dkt. Delila.
Akizungumzia kuhusu mkutano huo Dkt. Delila alisema lengo ni kuwapatia madaktari ujuzi hususani wa namna ya kupima moyo kwa kutumia mashine za ECHO na umeme wa moyo (Electrocardiography – ECG).
Kwa
upande wake Daktari kutoka hospitali ya Amana Natalius Kapilima alisema
mafunzo hayo yamewasaidia kupata ujuzi utakaowawezesha kuwatambua
wagonjwa wa moyo kupitia vipimo vya ECHO na ECG.
Naye
Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka hospitali ya Aga Khan Prof.
Mustafa Bapuma aliishukuru Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete kwa kuona
mbali na kuwezesha kufanyika kwa
mafunzo hayo kwa madaktari. Kupitia mafunzo hayo wataweza kutibu
wagonjwa wa moyo kwa ustadi na ufanisi zaidi kuliko hapo awali.
Mkutano huo wa siku moja umeandaliwa na Taasisi
ya Moyo Jakaya Kikwete kwa kushirikiana na Kampuni ya Merck ambapo
jumla ya washiriki 80 kutoka Hospitali mbalimbali za mkoa wa Dar es
Salaam walishiriki.
No comments :
Post a Comment