Tuesday, June 19, 2018

FURAHA YANGU MAANDALIZI YA UFUNGUZI 19 JUNE 2018 JIJINI DODOMA


pic 1 (1)
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Watu wenye Ulemavu) Mhe Jenista Mhagama (wa pili kushoto) akiwa ameandamana na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt Bilinith Mahenge (kushoto),  Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Prof Faustin Kamuzora (wa pili kulia), Mkurugenzi Mtendaji wa TACAIDS Dk Leonard Maboko (kulia) wakijadili jambo wakati wa ukaguzi wa maandalizi ya uzinduzi wa Kampeni ya Kitaifa ya Kupima VVU na kuanza kutumia dawa mapema inayojulikana kama Furaha Yangu. Kampeni  hiyo inatarajiwa kuzinduliwa rasmi kesho na Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa katika viwanja vya Jamhuri jijini Dodoma.
pic 2
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Watu wenye Ulemavu) Mhe Jenista Mhagama (wa pili kulia) akipokea maelezo kuhusu maandalizi ya uzinduzi wa Kampeni ya Kitaifa ya Kupima VVU na kuanza kutumia dawa mapema inayojulikana kama Furaha Yangu wakati alipotembelea uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma ambapo kampeni  hiyo inatarajiwa kuzinduliwa rasmi kesho na Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa.
PIC 3
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Watu wenye Ulemavu) Mhe Jenista Mhagama (wa kwanza kulia) akikagua mabanda ambayo yatatumiwa na wananchi kupima VVU  katika Kampeni ya Kitaifa ya Kupima VVU na kuanza kutumia
dawa mapema inayojulikana kama Furaha Yangu. Kampeni hiyo inatarajiwa kuzinduliwa rasmi kesho na Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa katika viwanja vya Jamhuri jijini Dodoma. Mhe Mhagama alikuwa ameandamana na kamati ya maadalizi wakiwemo Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt Bilinith Mahenge,  Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Prof Faustin Kamuzora pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa TACAIDS Dk Leonard Maboko.
………………..
MAELEZO YA KAMPENI YA KITAIFA YA KUPIMA VVU NA
KUANZA ARV MAPEMA
“FURAHA YANGU – PIMA, JITAMBUE, ISHI”
Utangulizi
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kupitia Mpango wa Taifa wa Kudhibiti UKIMWI kwa kushirikiana  na FHI360 mradi wa USAID –Tulonge Afya na wadau wengine inatarajia kufanya kampeni ya Kitaifa ya Upimaji wa VVU na Kuanza Kutumia ARV Mapema. Kampeni hii inasimamiwa na kikosi kazi kilichoundwa kwa kujumuisha wataalamu toka Wizara yetu, TACAIDS, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi na wadau wa VVU na UKIMWI. Jukumu kuu la kikosi kazi ni kusimamia maandalizi, utekelezaji na tathimini ya kampeni ikiwemo  kupitia matangazo na machapisho mbalimbali. Kamati hii inaongozwa na wenyeviti ambao NACP na TACAIDS, wakishirikiana na wawakilishi wa TAMISEMI, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma na kazi za kuweka kumbukumbu zimeongozwa FHI360 Kupitia mradi wa USAID Tulonge Afya.
Hali hali halisi ya maambukizi nchini
Utafiti wa nne uliofanyika katika ngazi ya kaya kuanzia mwezi Oktoba 2016 hadi Agosti 2017 ulibainisha kuwa wastani wa kitaifa wa maambukizi ya VVU kwa watu wenye umri wa miaka 15 hadi 49 ni asilimia 4.7. Wanawake ni asilimia 6.2 na wanaume ni asilimia 3.1.
Nchi yetu imeridhia na kuanza utekelezaji wa kauli mbiu ya kidunia ya TISINI TATU ifikapo 2020 (asilimia 90 ya watu wanaoishi na VVU wawe wamejua hali zao za maambukizo; asilimia 90 ya waliopimwa VVU na kugundulika kuwa wana maambukizo wapatiwe dawa za kufubaza makali ya VVU; na asilimia 90 ya watu wanaotumia dawa wawe wamefubaza VVU). Hali halisi ya utekelezaji wa kufikia hizi tisini tatu ni Kama ifuatavyo:
Tisini ya Kwanza: Nchini Tanzania ni asilimia 52.2 tu ya wanaoishi na VVU wenye umri wa miaka 15 – 64 walitoa taarifa kuwa wanajua hali zao za maambukizo ya VVU (Wanawake  ni asilimia 55.9 na Wanaume  ni asilimia 45.3)
Tisini ya Pili: Kati ya watu wanaoishi na VVU wenye umri wa miaka 15 – 64 ambao wanajua hali zao za maambukizo, asilimia 90.9 walitoa taarifa kuwa wanatumia dawa za kufubaza VVU (Wanawake  ni asilimia 92.9 na Wanaume ni asilimia 86.1)
Tisini ya Tatu: Kati ya watu wanaoishi na VVU wenye umri wa miaka 15 – 64 ambao wametoa taarifa kuwa wanatumia dawa za kufubaza VVU, asilimia 87.7 ya watu hao inaonyesha kiasi cha VVU kimefubazwa (Wanawake  ni asilimia 89.2 na Wanaume ni asilimia 84)
Hivyo basi, Tanzania inafanya vizuri sana katika Tisini ya pili na tatu, lakini tatizo kubwa ni katika kufikia 90 ya kwanza, kwani ni asilimia 52.2 tu ya wenye VVU wanajua hali zao. Tatizo hili ni kubwa zaidi miongoni mwa wanaume, kwani ni asilimia 45.3 tu ya wanaume wanaoishi na VVU wanajua hali zao.
Jina la Kampeni
Kampeni hii inaitwa “Furaha Yangu” na itafuatiwa na kauli mbiu “tagline” Pima, Jitambua, Ishi Jina na kauli mbiu vimejaribiwa kwa wataalamu na walengwa na kuchaguliwa kati ya majina na kauli mbiu tatu zilizopendekezwa toka kauli mbiu tano na majina matano ya awali.
Madhumuni ya Kampeni
Madhumini ya kampeni hii ni kufikia malengo ya Tanzania kwamba ifikapo mwaka 2020 asilimia 90 ya watu wanaoishi na VVU wanatambua hali zao za maambukizi, asilimia 90 kati yao wanatumia ARV na asilimia 90 ya wanaotumia ARV kiwango chao cha VVU mwilini kinashuka.
Malengo
Malengo ya kampeni ni kusaidia kutimiza malengo ya Tisini tatu (90 90 90) kwa kuzingatia malengo yaliyowekwa Kitaifa na Mikoa. Hasa katika mikoa  ya utekelezaji wa mradi wa Tulonge Afya (Upande wa Uhamasishaji) na Boresha Afya (Upande wa Utoaji wa Huduma) ambayo ni Arusha, Kagera, Geita, Shinyanga, Kigoma,  Mara, Mwanza, Tabora, Singida, Iringa, Njombe,  Mtwara, Morogoro, Lindi, Ruvuma, Dodoma Kilimanjaro, Manyara na Simiyu.
Walengwa wa Kampeni
Walengwa wa kampeni hii ni kama wafuatavyo:
Walengwa wa Msingi / Kwanza
  • Watu ambao hawajawahi kupima VVU na wako katika Hatari ya kumbukizwa au kuambukiza VVU:
    • Wanaume wenye Umri chini ya Miaka 45
    • Wasichana walio katika umri wa balehe
    • Wanawake wenye umri wa miaka 15-24
    • Akinamama wajawazito
  • Watu ambao wameambukizwa VVU na hawajaanza kutumia ARV
  • Akina Mama wanaoishi na VVU na Wananyonyesha pamoja na watoto wao
Walengwa wa Pili
  • Familia na wale wanaomsaidia mlengwa wa kwanza ikijumuisha watu wenye ushawishi katika jamii na viongozi serikari na viongozi wa dini
  • Watoa huduma za afya ngazi ya kituo na jamii
Njia  za Mawasiliano
  • Radio za Kitaifa
  • Radio za Mikoa au Kijamii
  • Mitandao ya Kijamii
  • Televisheni
  • Watoa huduma za Afya na walielimisharika – Mawasiliano ya ana kwa ana
  • Machapisho ya aina mbalimbali
  • Mikutano ya ulaghabishi Kitaifa, Mikoa na Wilaya
Huduma kwa walengwa
Huduma za upimaji wa VVU na kuwaunganisha katika huduma za tiba na matunzo wateja watakaokuwa wameambukizwa VVU zitatolewa na Mikoa  kwa kushiriana na wadau katika Vituo vya Huduma za Afya, huduma ngazi ya jamii na maeneo ya kazi kwa lengo la kuwafikia wanaume na vijana wengi.
Ufuatiliaji na Tathimini
  • Kwa sasa kuna kampuni ya kangaroo media ambayo inatengeneza matangazo yote na itafuatilia mitandao ya kijamii kupitia IPSOS
  • Matangazo ya Redio na Televisheni ufuatiliaji wake utafanyia kwa kampuni ambayo itachaguliwa
  • Takwimu nyingine zitafuata mfumo uliopo
Uzinduzi
  • Kampeni inatarajiwa kuzinduliwa 19/06/2018 mkoani Dodoma ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mhe.Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Majaliwa Kassim Majaliwa.
  • Kabla ya uzinduzi tunatarajia kuwa na kikao na waandishi wa habari 12 Juni 2018 ambapo wananchi kupitia wanahabari watapewa taarifa kuhusu uzinduzi wa kampani na ushiriki wa Mh.Waziri Mkuu. Aidha, matarajio yetu ni kupata Ushiriki wa  Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mh. Ummy Mwalimu (Mb), na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Watu wenye Ulemavu, Mhe. Jenista Mhagama (Mb), Waziri wa nchi ofisi ya Raisi  Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mh. Selemani Saidi Jafo (Mb), Mkurugezi wa Tiba, Mkurugenzi wa Kinga, Meneja Mpango, Mkurugenzi Mtendaji wa TACAIDS, Mwakilishi wa USAID, mwakilishi wa ILO na wadau wengine.
  • Tunatarajia kufanya shughuli za upimaji wa afya ngazi ya jamii Jijini Dodoma kuanzia tarehe 18/06/2018 hadi siku ya uzinduzi 19/06/2018.
  • Baada ya uzinduzi wa kitaifa tunatarajia kuwa na uzinduzi katika ngazi za kanda na mikoa Tukianza na mikoa ya Njombe, Iringa, Tabora, Mwanza na Shinyanga.
Ufadhili
Kampeni hii inaufadhili wa wadau watatu hadi sasa:-
  • Serikali kupitia Wizara  ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto na TAMISEMI
  • USAID kupitia mradi wa miaka mitano wa FHI360-Tulonge Afya (Uhamasishaji)
  • TACAIDS na ILO kipengele  cha kufikia wanaume wenye umri zaidi ya miaka 45, huu ni udhamini wa muda wa miezi sita

No comments :

Post a Comment