Waziri wa Fedha na Mipango Mhe.
Dkt. Philip Isdor. Mpango (Mb) (kushoto) na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki
ya NMB Bi. Ineke Bussemaker, wakipeana mkono wakati wa makabidhiano ya
hundi kifani yenye thamani ya shilingi bilioni 10.1, ambayo ni gawio
lililotolewa na Benki ya NMB kwa Serikali, Jijini Dodoma.
(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Fedha na Mipango)
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe.
Dkt. Philip Isdor. Mpango (Mb) (kushoto) na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki
ya NMB Bi. Ineke Bussemaker, wakiangalia hundi kifani yenye thamani ya
shilingi bilioni 10.1, ambayo ni gawio lililotolewa na Benki ya NMB kwa
Serikali, Jijini Dodoma.
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe.
Dkt. Philip Isdor. Mpango (Mb) (wa sita kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa
Benki ya NMB Bi. Ineke Bussemaker (wa saba kushoto) na Maafisa
waandamizi kutoka Benki ya NMB na Wizara hiyo wakiwa katika picha ya
pamoja baada ya
Serikali kupokea gawio la Sh. bilioni 10.1 kutoka NMB,
Jijini Dodoma.
………………………………………………………………….
Na Benny Mwaipaja, WFM, Dodoma
Benki ya NMB imetoa gawio la Sh.
bilioni 10.1 kwa Serikali ambayo inamiliki asilimia 32 ya hisa za Benki
hiyo baada ya kupata faida ya Sh. bilioni 94.8 baada ya kodi kwa mwaka
2017/2018.
Tukio hilo la kukabidhi hundi
kifani ya gawio hilo limefanyika Makao Makuu ya Wizara ya Fedha na
Mipango, Jijini Dodoma, kati ya Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt.
Philip Mpango, kwa niaba ya Serikali, na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki
hiyo Ineke Bussemaker.
Dkt. Mpango amezipongeza juhudi
za watendaji wa Benki hiyo waliofanikisha kupatikana kwa faida
iliyowezesha Serikali kupata gawio licha ya changamoto zilizoikumba
Sekta ya Benki likiwemo suala la mikopo chechefu.
“Mikopo chechefu imekua tatizo
kwa Benki nyingi nchini hivyo ninatoa rai kwa Benki ya NMB kuhakikisha
inafuata taratibu za kukopesha na kuendelea kusimamia vizuri wakopaji
ili kuondoa tatizo la mikopo chechefu” alieleza Dkt. Mpango.
Aidha ameipongeza Benki hiyo kwa
kutoa huduma katika Sekta ya kilimo na kuitaka ipanue wigo zaidi na
kuziwezesha sekta za uvuvi na ufugaji kutokana na umuhimu wake katika
ukuaji wa uchumi wa taifa.
Alisema kuwa anatarajia Benki
hiyo itatoa gawio zaidi mwaka ujao wa fedha na amemwagiza Msajili wa
Hazina, kuzihakiki taasisi zote ambazo Serikali imewekeza hisa zake ili
zitoe gawio lasivyo ametishia Serikali kuondoa hisa zake kwakuwa
uwekezaji huo hautakuwa na tija.
Kwa upande wake Mkurugenzi
Mtendaji wa Benki hiyo Ineke Bussemaker alieleza kuwa licha ya Benki
yake kutoa gawio hilo la shilingi bilioni 10.1 kwa Serikali, pia inalipa
kodi za Serikali vizuri ambapo katika kipindi cha mwaka 2017/18 imetoa
kodi ya shilingi bilioni 127.
Aliongeza kuwa tangu mwaka 2014
hadi 2017 benki hiyo imetoa kodi zinazofikia zaidi ya shilingi bilioni
460 na kwamba itaendelea kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma za kibenki
ili iweze kupata faida na kulipa gawio kubwa zaidi kwa wana hisa wake
ikiwemo Serikali inayomiliki silimia 31.8 ya hisa 500.
Aidha, amesema kuwa Benki yake
imeendelea kufanya kazi kwa karibu na Sekta ya Kilimo kwa kutoa huduma
za kifedha kwa wakulima wakiwemo wakulima wa Tumbaku na Korosho katika
mikoa ya Kusini ya Lindi na Mtwara, ambapo imefungua zaidi ya akaunti
300,000 na kuweza kukusanya zaidi ya shilingi bilioni 250 mwezi Novemba
mwaka jana.
Bi. Bussemaker alisema kuwa Benki
yake inajitahidi kuhakikisha kunakua na huduma jumuishi za kifedha kwa
wananchi kote nchini kwa kuweka Mawakala na kuongeza Matawi ya Benki
hiyo na pia kuhamasisha wananchi wafungue Akaunti ya Benki hiyo.
Alisema kuwa ili kufanikisha
utoaji wa huduma hiyo ya kifedha kwa watanzania, Benki hiyo imejipanga
kutumia teknolojia ya kisasa ya masuala ya fedha ambayo itarahisisha
kuwafikia watu wengi ikiwemo huduma za fedha kwa njia ya simu za
mkononi.
Katika Mwaka wa Fedha 2016/2017,
Benki hiyo ilitoa gawio la shilingi bilioni 16.5 kwa Serikali, huku
kukiwa na pungufu ya shilingi bilioni 6 mwaka huu hatua iliyomlazimu
Dkt. Mpango kuiagiza Benki hiyi ihakikishe inaboresha huduma zake ili
Serikali ipate gawio kubwa zaidi kwa ajili ya kutumia fedha hizo
kuwaletea wananchi maendeleo katika sekta za maji, afya, elimu, na
miundombinu mingine muhimu.
No comments :
Post a Comment