Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na
Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, akifafanua jambo wakati wa Siku ya
Maadhimisho ya Hali ya Hewa Duniani, mkoani Dodoma, kushoto ni Naibu
Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Eng. Atashasta Nditiye, wa pili Kulia
ni Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini (TMA), Dkt. Agness
Kijazi na kulia ni Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Nchini
(TCAA), Hamza Johari.
………………….
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na
Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa amesema Serikali itaendelea
kuiwezesha Mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini (TMA) kuwa na vifaa na mitambo
ya
kisasa ya hali ya hewa ili kuwezesha huduma bora za utabiri kutolewa
kwa wakati na usahihi kwa manufaa ya taifa.
Profesa Makame Mbarawa amesema
hayo mjini Dodoma leo wakati Tanzania ikiungana na nchi nyingine duniani
kuadhimisha Siku ya Hali ya hewa, na kusisitiza kuwa kwa sasa TMA
imeongeza imani kwa wananchi kwani imekuwa ikitoa utabiri wa kuaminika
kwa sababu ya kuwa vifaa vingi na vya kisasa vya utoaji taarifa.
“Nipende kuwahakikishia kuwa
Serikali itaendelea kuwezesha TMA na kuhakikisha kuwa inatoa utabiri
ambao ni sahihi na wa uhakika kwani kuwepo kwa utabiri sahihi
kutawezesha vyombo husika kuchukua hatua mapema kabla ya madhara makubwa
kutokea” amesema Waziri Prof. Mbarawa.
Waziri Prof. Mbarawa amewataka
wananchi kutunza mazingira kwa kuacha kulima kwenye vyanzo vya maji na
kuepuka kuchafua maeneo ya bahari ili kuepusha athari zinazoepukika
zikiwemo uharibifu wa miundombinu ya uchukuzi.
“Niwaombe wananchi wote watunze
mazingira kwani kumekuwa na uharibifu mkubwa wa miundombinu kutokana na
shughuli zinazofanywa na binadamu katika maeneo mbalimbali yasiyotakiwa
kulimwa au kujengwa, amesisitiza Waziri Prof. Mbarawa.
Kwa Upande wake Mkurugenzi Mkuu wa
TMA, Dkt. Agnes Kijazi ameishukuru Serikali kwa jitihada inazozifanya
kuwekeza kwenye miundombinu ya hali ya hewa kwa kutoa fedha kununua
vifaa mbalimbali ambavyo vimewezesha mamlaka hiyo kutoa utabiri
uliosahihi kwa zaidi ya asilimia 70.
Dkt Kijazi ameongeza kuwa kwa sasa
taarifa za hali ya hewa hasa kwenye usafiri wa anga zimeimarika ambapo
hutolewa kila baada ya nusu saa na kuwawezesha watumiaji wa usafiri huo
kupata taarifa kabla ya kuanza safari zao.
“Kwa sasa utabiri wa usafiri wa
anga ni wa uhakika mpaka asilimia 90 na hutolewa kila baada ya nusu saa
na marubani hupata taarifa hizo kwa wakati kabla ya kuanza safari zao,
amesema Dkt. Kijazi.
Siku ya Hali ya Hewa duniani
huadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 23 Machi ambapo mwaka huu
yanaongozwa na kauli mbinu isemayo “JIWEKE TAYARI NA ZINGATIA TAARIFA ZA HALI YA HEWA”.
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.
No comments :
Post a Comment