Friday, March 23, 2018

SERIKALI KUWEKEZA HALI YA HEWA-PROF. MBARAWA


1
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, akifafanua jambo wakati wa Siku ya Maadhimisho ya Hali ya Hewa Duniani, mkoani Dodoma, kushoto ni Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Eng. Atashasta Nditiye, wa pili Kulia ni Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini (TMA), Dkt. Agness Kijazi na kulia ni Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Nchini (TCAA), Hamza Johari.
………………….
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa amesema Serikali itaendelea kuiwezesha Mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini (TMA) kuwa na vifaa na mitambo ya
kisasa ya hali ya hewa ili kuwezesha huduma bora za utabiri kutolewa kwa wakati na usahihi kwa manufaa ya taifa.
Profesa Makame Mbarawa amesema hayo mjini Dodoma leo wakati Tanzania ikiungana na nchi nyingine duniani kuadhimisha Siku ya Hali ya hewa, na kusisitiza kuwa kwa sasa TMA imeongeza imani kwa wananchi kwani imekuwa ikitoa utabiri wa kuaminika kwa  sababu ya kuwa vifaa vingi na vya kisasa vya utoaji taarifa.
“Nipende kuwahakikishia kuwa Serikali itaendelea kuwezesha TMA na kuhakikisha kuwa inatoa utabiri ambao ni sahihi na wa uhakika kwani kuwepo kwa utabiri sahihi kutawezesha vyombo husika kuchukua hatua mapema kabla ya madhara makubwa kutokea” amesema Waziri Prof. Mbarawa.
Waziri Prof. Mbarawa amewataka wananchi kutunza mazingira kwa kuacha kulima kwenye vyanzo vya maji na kuepuka kuchafua maeneo ya bahari ili kuepusha athari zinazoepukika zikiwemo uharibifu wa miundombinu ya  uchukuzi.
“Niwaombe wananchi wote watunze mazingira kwani kumekuwa na uharibifu mkubwa wa miundombinu kutokana na shughuli zinazofanywa na binadamu katika maeneo mbalimbali yasiyotakiwa kulimwa au kujengwa, amesisitiza Waziri Prof. Mbarawa.
Kwa Upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dkt. Agnes Kijazi ameishukuru Serikali kwa jitihada inazozifanya kuwekeza kwenye miundombinu ya hali ya hewa kwa kutoa fedha kununua vifaa mbalimbali ambavyo vimewezesha mamlaka hiyo kutoa utabiri uliosahihi kwa zaidi ya asilimia 70.
Dkt Kijazi ameongeza kuwa kwa sasa taarifa za hali ya hewa hasa kwenye usafiri wa anga zimeimarika ambapo hutolewa kila baada ya nusu saa na kuwawezesha watumiaji wa usafiri huo kupata taarifa kabla ya kuanza safari zao.
“Kwa sasa utabiri wa usafiri wa anga ni wa  uhakika mpaka asilimia 90 na hutolewa kila baada ya nusu saa na marubani hupata taarifa hizo kwa wakati kabla ya kuanza safari zao, amesema Dkt. Kijazi.
Siku ya Hali ya Hewa duniani huadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 23 Machi ambapo mwaka huu yanaongozwa na kauli mbinu isemayo “JIWEKE TAYARI NA ZINGATIA TAARIFA ZA HALI YA HEWA”.
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.


No comments :

Post a Comment