Akizungumza
kama mmojawapo wa jopo la wazungumzaji wakati wa semina hiyo, Mkuu wa
Kitengo cha Masoko wa Jumia Tanzania, kampuni ambayo inajihusisha na
biashara ya manunuzi na uuzaji wa bidhaa mtandaoni, Bw. Albany James
amesema kuwa changamoto kubwa wanayopambana nayo kwa sasa ni kuhakikisha
kwamba inawashawishi wafanyabiashara wote kuhamia kwenye mfumo wa
mtandaoni ili kuwafikia wateja wengi zaidi.
“Kikubwa
tunachokifanya ni kuwakutanisha wauzaji wa bidhaa mbalimbali na wateja
mtandaoni. Kupitia uwekezaji mkubwa wa teknolojia tulioufanya,
tumedhamiria kuwapatia wauzaji na wanunuaji urahisi mkubwa sawasawa na
kama wanavyokwenda madukani,” alisema na kuhitimisha Bw. James,
“Tunafahamu kwamba kwenye biashara ili kufikia soko kwa urahisi ni
lazima uwajue wateja wako na namna ya kuwafikia ambapo mara nyingi ni
kwa njia ya matangazo.
SOMA ZAIDI »
Lakini
sio wafanyabiashara wote wanaweza kulimudu ukizingatia wengi ndio
wanaanza na hawana mitaji au faida kubwa ya kuwekeza kwenye matangazo.
Hivyo basi, Jumia tunachokifanya ni kuwapatia fursa ya kujitangaza kwa
njia ya mtandao bila ya gharama yoyote kwani ndipo kwenye idadi kubwa ya
watu kwa hivi sasa.”
Naye kwa
upande wake Meneja Uhusiano wa Umma na Masoko wa Jumia Travel Tanzania,
Bw. Kijanga Geofrey, kampuni dada ya Jumia Tanzania ambayo yenyewe
inajihusisha na utoaji wa huduma za hoteli mtandaoni nchini na barani
Afrika kwa ujumla, ameongezea kuwa fursa iliyopo kwa wafanyabiashara
kuhamia mtandaoni ni kubwa na haina gharama kama wengi wanavyofikiri.
“Wafanyabishara
wengi bado ni waoga wa kutumia teknolojia kwenye kukuza na kurahisisha
biashara zao. Ripoti zinaonyesha kwamba Tanzania ni mojawapo ya nchi 20
zenye uchumi unaokua kwa kasi duniani ambao kwa kiasi kikubwa
unachangiwa na sekta za utalii, ujenzi, fedha na biashara ukiacha na
nyinginezo. Lakini kikubwa zaidi ni ukuaji wa TEHAMA ambapo takwimu
zinaonyesha 40% ya watanzania wamefikiwa na mtandao wa intaneti ambapo
wameongezeka na kufikia milioni 19.86 mwaka 2016 kutoka milioni 17.26
mwaka 2015. Takwimu hiyo pia imechochea kuongezeka kwa watumiaji wa simu
za mkononi na kufikia milioni 40.17 mwaka 2016,” alisema Bw, Geofrey.
“Hilo ni
sawa na ongezeko la 0.9% kwa mwaka na ukuaji wa ueneaji kwa 83% kwenye
nchi yenye idadi ya watu zaidi ya milioni 50. Hii ni dhahiri kwamba kuna
mustakabali mkubwa kwa ukuaji wa biashara za mtandaoni kwenye sekta
mbalimbali. Kwa sasa mawasiliano ya simu ni mojawapo ya sekta zinazokua
kwa kasi nchini Tanzania na inatoa mchango mkubwa katika kuwaunganisha
watanzania kwenye mfumo wa kifedha. Kwa kuongezea, idadi ya watumiaji wa
huduma za fedha kwa njia ya simu nayo imeongozeka na kufikia milioni
18.08 mwaka 2016 kutoka milioni 17.63 mwaka 2015. Hizi zote ni ishara
kwamba watanzania wapo tayari kwa biashara za mtandaoni kitaalamu na
kisaikolojia,” alihitimisha Meneja huyo wa Uhusiano wa Umma na Masoko wa
Jumia Travel Tanzania.
No comments :
Post a Comment