Saturday, November 18, 2017

WAGONJWA 33 WAFANYIWA UPASUAJI MOYO WA BILA KUFUNGUA KIFUA (CATHETERIZATION) KWA KUTUMIA MSHIPA WA DAMU WA MKONO KATIKA KAMBI MAALUM YA MATIBABU


Picha no. 3
Madaktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Taasisi ya Kimataifa ya Kiislamu ya  Misaada (IIRO) ya nchini Saudi  Arabia wamefanya upasuaji wa kuzibua mishipa ya moyo kupitia mshipa wa damu wa mkono (Catheterization) kwa kutumia mtambo wa Cathlab kwa wagonjwa 33.
Kwa mara ya kwanza tangu Taasisi imeanza  kutoa huduma ya matibabu ya upasuaji wa Moyo bila ya kufungua kifua tumefanya  upasuaji wa kuzibua mishipa ya moyo kupitia mshipa wa damu wa mkono. Upasuaji tuliokuwa tunaufanya kwa wagonjwa wetu ni wa kutumia mishipa ya paja.
Upasuaji wa moyo unaofanyika katika kambi hii ambayo imeanza Jumatano tarehe 15/11/2017 hadi Jumamosi tarehe 18/11/2017 ni ya upasuaji wa bila kufungua kifua kwa watu wazima. Upasuaji uliofanyika  ni wa kuzibua mishipa ya moyo iliyoziba.
Faida ya upasuaji uliofanyika ni  kumwezesha mgonjwa kutoka ...
chumba cha upasuaji akiwa  anatembea na baada ya masaa manne kama hali yake inaendelea vizuri anaweza kuruhusiwa. Tofauti na upasuaji wa kutumia mshipa wa paja ambao tulikuwa tunaufanya, baada ya upasuaji mgonjwa ni lazima akae Hospitali kwa zaidi ya masaa 24 ili kuangalia maendeleo ya afya yake.
Kambi hii imeenda  sambamba na utoaji wa elimu na kubadilishana ujuzi wa kazi  kati ya wafanyakazi wa Taasisi hizi mbili ikiwemo aina mpya ya upasuaji uliofanyika kitu ambacho kimewajengea uwezo zaidi wafanyakazi wetu.  Aidha wageni nao wamepata muda wa kujifunza vitu vingi na kupata uzoefu mpya  wa baadhi ya magonjwa na mambo ya kiteknolojia ambayo katika nchi yao hakuna.
Tunaendelea kuwasisitiza wananchi kujenga tabia ya kupima afya zao mara kwa mara hii itawasaidia kujuwa kama wana matatizo ya moyo au la na hivyo kupata tiba kwa wakati. Changamoto  kubwa tunayokabiliana  nayo katika matibabu ya wagonjwa wetu ni wagonjwa wengi tunaowapokea mioyo yao kutokuwa katika hali nzuri.
Kama mnavyofahamu matibabu ya moyo ni ya gharama hivyo basi tunaendelea kuwahimiza wananchi  kujiunga na mfuko wa taifa wa bima ya afya ambao utawasaidia kulipa gharama za matibabu pindi  watakapougua na kuhitaji kupata matibabu.
Kwa namna ya kipekee tunaishukuru sana  Taasisi ya Kimataifa ya Kiislamu ya  Misaada (IIRO) kwa kutuma wataalam wake wa magonjwa ya moyo kuja hapa nchini kutoa huduma ya matibabu kwa wagonjwa wetu.

No comments :

Post a Comment