Waziri wa AfYa Mahmoud Thabiti
Kombo akimkaribisha Daktari bingwa wa maradhi ya moyo Duniani Dkt
Ramakanta Panda alipomtembelea Ofisini kwake Mnazimmoja Zanzibar kuhusu
kambi wanayotarajia kuifanya ya matibabu ya Moyo mwezi June.
Daktari bingwa wa maradhi ya moyo
Duniani Ramakanta Panda kutoka Taasisi ya Moyo ya Asia akizungumza na
waandishi wa habari hawapo pichani Wizara ya Afya kuhusu Kambi ya
Matibabu ya Moyo inayotarajiwa kufanywa na Taasisi hiyo kwa kushirikiana
na Wizara ya Afya mwezi June. Kushoto yake ni Waziri wa Afya Mahmoud
Thabit Kombo.
Picha na Abdalla Omari-Habari Maelezo Zanzibar
……………..
Na Faki Mjaka-Maelezo Zanzibar
Kufuatia ongezeko la maradhi ya
moyo Zanzibar Taasisi ya Moyo ya Asia yenye makao yake nchini India kwa
kushirikiana na Wizara ya Afya Zanzibar inatarajia kuweka Kambi ya
Matibabu ya Moyo kwa kipindi cha wiki moja.
Kambi hiyo inatarajiwa kuanza
mwezi wa Juni ambapo Wataalam wa Tiba za Moyo watakuja na kufanya
uchunguzi wa afya kwa Wananchi wa Zanzibar.
Akizungumza na Waandishi wa habari
Waziri wa Afya wa Zanzibar Mahmoud Thabit Kombo amesema kwa wastan
Wizara ya Afya inapokea wagonjwa wa Moyo 160 hadi 180 kwa mwaka.
Amesema idadi hiyo ni ya Wananchi
ambao hujitokeza kwa hiari kupima afya zao na kwamba kuna uwezekano
idadi kuongezeka siku hadi siku.
“Hawa wagonjwa 160-180
tunaowabaini na maradhi ya moyo ni wale tu ambao wamekuja kupima
inawezekana ikawa kuna idadi kubwa ya wagonjwa ambao bado hawajaenda
Hospital kupima afya zao” alisema Waziri Kombo.
Waziri Kombo amesema wagonjwa
watakaobainika na maradhi ya Moyo watafanyiwa matibabu na wale
watakaolazimika kufanyiwa upasuaji watapewa maelekezo ya wapi waafanyiwe
upasuaji.
Amesema nchini India wagonjwa
wengi hawalazimiki kufanyiwa upasuaji badala yake hupatiwa Dawa kwa vile
tu wanawahi mapema kufanyiwa uchunguzi wa kiafya.
Hivyo Waziri huyo amewaomba
wananchi kujitokeza kwa wingi kupima afya zao kwa wastani wa mara moja
kwa mwezi ili kujiweka katika mazingira mazuri kiafya.
Kwa upande wake Daktari Bingwa wa
Moyo kutoka Taasisi ya Moyo ya Asia Ramakanta Panda amesema kwa kipindi
cha mwaka Taasisi yao itatuma timu ya wataalam wa maradhi ya Moyo kuja
Zanzibar kufanya kambi mara mbili kwa lengo la kukagua afya za Wagonjwa
wa Moyo Unguja na Pemba.
Mbali na Kambi, Taasisi hiyo
imekubali kuwasomesha Madaktari wawili kutoka Zanzibar ambao wataenda
nchini India kujifunza zaidi kuhusu maradhi ya Moyo kwa kipindi cha
mwaka mmoja.
Dkt. Panda amesema yupo tayari
kushirikiana moja kwa moja na Serikali ya mapinduzi ili kusaidia ujenzi
wa kituo cha matibabu ya Moyo maeneo ya Binguni Wilaya ya Kusini Unguja.
Aidha Waziri Kombo amemuonesha
Dkt. Bingwa huyo michoro mbali mbali ya kituo cha Taasisi ya Moyo
Zanzibar ambacho kitasaidia pakubwa katika mapambano dhidi ya maradhi ya
Moyo.
Madakatari hao watakuja kufanya
uchunguzi wa Moyo kwa wananchi mbali mbali kupitia vifaa mbali mbali na
kutoa ushauri wa kitaalamu namna bora ya kujikinga na maradhi mbalimbali
ikiwemo Moyo.
IMETOLEWA NA MAELEZO ZANZIBAR
No comments :
Post a Comment