Saturday, November 18, 2017

SIKU YA TAKWIMU AFRIKA KUADHIMISHWA KESHO


PICHA 1
Mkurugenzi wa Shughuli za Kitakwimu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Irenius Ruyobya akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) hivi karibuni kuhusu maadhimisho ya Siku ya Takwimu Afrika yatakayofanyika kesho tarehe 20 Novemba, 2017 katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es Salaam.
…………………………………………………………..
Na: Veronica Kazimoto-Dar es Salaam,
Maadhimisho ya Siku ya Takwimu Afrika yatafanyika kesho tarehe 20 Novemba, 2017 katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam hivi karibuni, Mkurugenzi wa Shughuli za Kitakwimu kutoka Ofisi ya Taifa ya...
Takwimu (NBS) Irenius Ruyobya alisema maadhimisho hayo yanayoratibiwa na ofisi hiyo kwa niaba ya Serikali, yana lengo la kuongeza ufahamu kuhusu nafasi na mchango wa Tasnia ya Takwimu katika kuleta maendeleo ya kiuchumi na kijamii Barani Afrika.
Ruyobya alisema kuwa kaulimbiu ya Siku ya Takwimu Afrika kwa mwaka huu ni “Takwimu Bora za Uchumi kwa Maisha Bora”
“Kaulimbiu hii inalenga kuweka mkazo katika matumizi ya Takwimu za Uchumi kwa ajili ya kuboresha maisha ya wananchi wote nchini na  Afrika kwa ujumla”, amebainisha Ruyobya.
Ruyobya alifafanua kuwa matumizi sahihi ya Takwimu za Uchumi yanaiwezesha Serikali kutunga sera na kutathmini programu mbalimbali kama vile Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (FYDP-II), Agenda ya Dunia ya Mwaka 2030 ya Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs) na Agenda ya Afrika ya Mwaka 2063.
“Progaramu zote hizi, zina lengo la kuboresha maisha ya wananchi kwa kuhakikisha kuwa, kuna upatikanaji wa Huduma za afya, Elimu, Miundombinu ya umeme na barabara, Mawasiliano, Utunzaji wa mazingira pamoja na Utawala bora”, amesema Ruyobya.
Jumla ya washiriki 200 kutoka katika Wizara, Idara na Taasisi za Serikali, Wadau wa Maendeleo, Vyuo vya Elimu ya Juu, Wanafunzi wa Shule za Sekondari pamoja na Wadau mbalimbali wa takwimu nchini wanatarajiwa kuhudhuria kwenye maadhimisho hayo.
Siku ya Takwimu Afrika huadhimishwa kila mwaka tarehe 18 Novemba ambapo kwa mwaka huu, Tanzania itaadhimisha siku hiyo kesho tarehe 20 Novemba, 2017.

No comments :

Post a Comment